728x90 AdSpace

­
Latest News
March 13, 2017

TAFAKARI YA SIKU: Jumanne, Juma la 2 la Kwaresima Mwaka A Tarehe 14/03/2017


Masomo:-

     Somo: Isa 1:10, 16-20

     Zab: 50: 8-9, 16bc-17, 21, 23

     Injili: Mt 23:1-12

Nukuu:

“Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteeni mjane,” Isa 1:16-17

“Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu,” Mt 23:8

TAFAKARI: “Utayari wa Mungu kusamehe; Yesu Kristo Mpatanishi wetu na Mungu na mwenye mamlaka ya kusamehe dhambi.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo tutafakari kwa pamoja “Utayari wa Mungu kusamehe; Yesu Kristo Mpatanishi wetu na Mungu na mwenye mamlaka ya kusamehe dhambi.” Ndugu yangu, mwito wa Nabii Isaya kwa watu wa Sodoma na Gomora, ni kuacha njia mbaya na kumrudia Mungu. Mungu yupo tayari muda wote kusamehe kwa sababu MSAMAHA ni moja ya uhasili wake.

Mungu daima ni, “mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha nne,” Kut 34:7.

Tendo la kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha nne, ni matokeo ya laana. Laana ni kinyume cha baraka. Kwa upande mwingine, laani huenda hadi kizazi cha nne. Kwa mantiki hiyo, yapo mambo fulani watu huteseka bila kujua, na chanzo chake yawezekana watu fulani, wakati fulani, hawakuenenda katika njia ya Bwana.

Kuepuka tatizo hilo, Nabii Isaya anawatahabarisha watu wa Sodoma na Gomora na kusema kwamba, “Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteeni mjane,” Isa 1:16-17

Ndugu yangu, upendo wa Mungu kwetu na utayari wake wa kusamehe hauna mfano. Kinachotokea kwa upende watu, ni kukubali kufa na tai shingoni, ni kwa sababu ya kiburi chetu. Chapa tulioyonayo ya sura na mfano wake Mungu, Mwa 1:27, ndiyo mvuto mkubwa wa hurama yake kwetu. Mungu wetu hapendi kuona tunaangamia bure. Anasema hata kama tungekuwa na dhambi nyekundu kama bendera, yupo tayari kusameha na kuzifanya nyeupe kama sufu, Isa 1:18.

Mpendwa, kwa nini unakubali kuumwa na mbwa aliyefungwa na kamba kwenye mti? Dhambi, ni kujipeleka ukijua kabisaaa! Wokovu ni kumrudia Muumba wako ukijua uzuri na wema wake. Hata hivyo, pamoja na madhaifu yetu, Mungu bado hajakata tamaa nasi.

Pamoja na watu kutokutambua wema wa Mungu, “ila wakakataa kutii, wala hawakuyakumbuka maajabu yako, uliyoyafanya kati yao; lakini wakafanya shingo zao kuwa ngumu, na katika kuasi kwao wakaweka jemadari, ili wairudie hali ya utumwa; lakini wewe u Mungu, uliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema, basi hukuwaacha,” Neh 9:17.

Ndugu yangu, watu wengi hujihukumu wenyewe na kujifungia neema za kupatanishwa na Mungu. Ni kosa kubwa kuishi katika hatia fulani. “Na kama mtu akifanya dhambi, na kutenda mambo hayo mojawapo ambayo Bwana alizuilia yasifanywe, ajapokuwa hakuyajua, ni mwenye hatia vivyo, naye atachukua uovu wake,” Wal 5:17. Lakini Mungu wetu hakai na hasira yake milele. Kufanya hivyo ni kinyume cha uhalisia wake. Yeye hufurahia rehema. “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema,” Mik 7:18.

Katika Injili yetu ya leo, Yesu anatoa angalizo kwa wanafunzi wake akisema wawe macho juu ya waandishi na mafarisayo kwa kujihesabia haki na kukaa katika kiti cha Musa. Wapendwa, Musa anawakilisha sheria. Mafarisayo na waandishi kukaa katika kitu cha Musa ni kuwa juu ya Sheria za Mungu. Wanajichukulia mamlaka yasiyo yao, na kuwabebesha watu mizigo mizito isiyo bebeka.

Ushauri wa Yesu kwetu kuhusu Mafarisayo na Waandishi, ni kutenda na kuisha wasemayo, ila kwa mfano wa matendo yao tusitende. Yesu Kristo anaona kasoro ya watu hawa na anawakemea kwa kusema, “ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie,” Mt 23:13. Wanausema na kuusifia utakatifu bila kuuishi.

Badala yake, Yesu anatutaka kufanya hili, “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu,” Mt 23:8. Mwalimu wetu ni Yesu Kristo, na katika Yeye sote kwa kupitia sakramenti ya Ubatizo tumerudishiwa urithi wetu na kuwa wana wa Mungu. Kwa tukio hili la kupatanishwa na Mungu Baba kupitia mwanaye Mpenzi Yesu Kristo, sisi sote leo ni ndugu. Kwa upatanisho huo, Yesu Kristo anayo mamlaka ya kusamehe dhambi. “Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6

Ndugu yangu, nani aliye tabibu zaidi ya Bwana wetu Yesu Kristo? Ni kwa Yesu Kristo tunaweza kuponywa na kuwa huru tukiwa na haja hiyo. “Na makutano walipojua walimfuata; akawakaribisha, akawa akisema nao habari za ufalme wa Mungu, akawaponya wale wenye haja ya kuponywa,” Lk 9:11. Je, mwenzangu humuitaji Yesu? Kuponywa huku na Yesu ni matokeo ya kuziungama dhambi na kuomba uponyaji huo. Tendo hili linatupelekea kuwa na haja ya kuponywa. “Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii,” Yak 5:16. Amina

Tumsifu Yesu Kristo!

“Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu,” Mt 23:8


Tusali:-Ee Yesu, usituache waja wako tunapoitaji uponyaji wako. Amina
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 blogger-facebook:

Post a Comment

Item Reviewed: TAFAKARI YA SIKU: Jumanne, Juma la 2 la Kwaresima Mwaka A Tarehe 14/03/2017 Rating: 5 Reviewed By: Unknown