728x90 AdSpace

­
Latest News
March 6, 2017

Mfahamu Mwasisi wa Jina la “TANZANIA” na jinsi alivyobuni jina hilo.


Na. James J. Waibina

Mpendwa Msomaji wetu wa Jarida la Fumbuka na BLOG yetu ya Fumbuka leo katika Makaa hii ya FAHAMU ninakuletea wasifu wa Mwasisi wa Jina la nchi yetu Tanzania pamoja na namna alivyobuni jina hilo.

Unapotaja historia ya nchi ya Tanzania, ni dhahiri kwamba hutaacha kutaja majina ya wapigania uhuru na viongozi mbalimbali walioiongoza tangu enzi za ukoloni, hadi kupata uhuru.

Hata hivyo, katika kila historia ya taifa lolote iliyojengwa, kuna watu waliofanikisha historia hiyo, lakini kwa sababu moja au nyingine, michango ya baadhi yao imesahaulika na pengine kutotajwa kabisa kwenye historia hizo.

Wengi wa Watanzania tunafahamu kuwa jina la nchi yetu Tanzania, limetokana na majina ya nchi mbili zilizoungana na kuwa moja ambazo ni Tanganyika na Zanzibar. Hivi ndivyo tulivyofundishwa shuleni.

Wengine wanaamini kuwa Rais wa kwanza na muasisi wa taifa hili, Hayati Mwalimu Julius Nyerere ndiye aliyebuni jina la Tanzania.

Lakini ukweli ni kwamba, jina la Tanzania lilibuniwa na mmoja wa wananchi walioshiriki mchakato wa kutafuta jina la nchi hii, baadaya muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.

Mohammed Iqbal Dar
 ndiye aliyebuni jina la Tanzania, wakati huo akiwa na umri wa miaka 18 akiwa mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Mzumbe.

Wasifu Wake:
Mohammed Iqbal Dar aliazaliwa miaka ya 1944 jijini Tanga, ni mtoto wa tatu kati ya watoto saba wa Mzee Tufail Ahmad Dar. Baba mzazi wa Mohammed alikuwa Daktari huko mkoani Morogoro alikuwa anaitwa Dr. T A DAR alihamia Tanganyika kutoka India mwaka 1930.

Mohammed Iqbal Dar alipata elimu yake ya Msingi Mkoani Morogoro shule ya Msingi H H D AGHAKHAN kwa sasa ni Shule ya Serikali na baada ya hapo alikuja baadae kujiunga na Chuo cha Mzumbe akasoma Kidato cha Kwanza mpaka cha Sita.

Ilikuwaje Akabuni Jina?
"Nilikuwa maktaba najisomea, nilishika gazeti la Daily News, wakati huo likiitwa The Standard, ndipo nikaona tangazo hilo," anaeleza Dar alivyopata hamasa na kuongeza:
"Siku hiyo hiyo, nikafanya majaribio ya kutafuta jina bila hata ya kuishirikisha familia yangu. Nilichukua karatasi na kalamu, lakini kabla sijaanza kufanya chochote, nilimwomba Mungu aniwezeshe kwa maana naamini Mungu, ndiye kila kitu wakati wa kufanya jambo lolote."

Jinsi Alivyopata Jina La Tanzania
“Kwa hiyo kwenye ile karatasi nikaandika Tanganyika na Zanzibar kisha, nikaandika majina yangu mawili, Iqbal na Ahmadiya,” anasema Dar na kufafanua kuwa Iqbal ni jina lake na jina la ubini na  Ahmadiyya ndiyo dhehebu lake. Alimwomba tena Mungu amsaidie ili apate jina zuri kutoka katika majina hayo aliyokuwa ameyaandika.  

Baada ya hapo Mohammed Iqbal Dar alichukua herufi tatu kutoka Tanganyika yaani TAN na kwa upande wa Zanzibar akachukua Herufi tatu za Mwanzo ZAN ukiunganisha unapataTANZAN alivyoona hivyo akachukua herufi ya kwanza katika jina lake la Iqbal na akachukua A kutoka jina la dini yake yaani Ahmadiyya kwa maana hiyo ukiongeza herufi hizi mbili na kwenye TANZAN unapata jina kamili TANZANIA.

Akalisoma jina akaliona ni zuri lakini akajiridhisha pia kwamba akiongeza herufi hizo za na kwenye TANZAN italeta maana kwakuwa nchi nyingi za Afrika zinaishia na IA, mfano EthiopIAZambIA, NigerIA, TunisIA, SomaLIA, GambIA, NamibIA, LiberIA, MauritanIA alivyoona hivyo akaamua apendekeze kuwa jinaTANZANIA ndio litumike kuwakilisha nchi hizi mbili yaani Tanganyika na Zanzibar kwa maana hiyo jina TANZANIA limezaliwa kutoka majina manne majina hayo ni TanganyikaZanzibar, Iqbal na Ahmadiyya.

Mohammed Iqbal Dar baada ya kupata jina hilo akalituma jina hilo kwenye kamati ya kuratibu Shindano. 

Baada ya muda mwingi kupita baba yake, mzee Tufail Ahmad Dar, alipokea barua kutoka Wizara ya Habari na Utalii (wakati huo), ambapo ndani yake kulikuwa na ujumbe wa pongezi ya kwamba kijana wake ameshinda katika shindano hilo.

"Wakati naandika, sikuwa na matumaini kama nitashinda kwa kuwa shindano hilo lilikua wazi kwa watu mbalimbali, hivyo sikuwa na tarajio lolote kama ningeshinda".


Barua ilisomeka hivi;-

“Utakumbuka kuwa miezi michache iliyopita ulituandikia kutupa ushauri kuhusu jina jipya la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na wewe pamoja na wananchi wenzio 16 ulishauri nchi yetu iitwe Tanzania.

“Nafurahi kukuarifu kuwa mshirikiane ile zawadi ya sh 200 iliyoahidiwa na leo nakuletea check ya sh 12/50 ikiwa ni hisa yako katika zile sh 200. Nashukuru sana kwa jitihada ya kufikiri jina la jamhuri yetu,” ilisema barua hiyo.

Sasa kwa nini Mohamed Iqbal Dar anadai kuwa mshindi pekee wakati barua ilionyesha kulikuwa na washindi wengine 15?

Anasema wakati wa kutolewa kwa zawadi hizo hakuna aliyejitokeza zaidi ya Mohammed Iqbal Dar na Yusufal Pir Mohamed ambaye hata hivyo alikosa sifa baada ya kushindwa kutoa barua ya pongezi ya kushinda kwa madai kuwa ameipoteza.

Hivyo Wizara ya Habari na Utalii iliamua kumtangaza Iqbal Dar kuwa mshindi na kumpatia zawadi yote ya sh 200 pamoja na ngao.
Iqbal Dar anasikitika mchango wake kutotambuliwa ingawa anaipenda Tanzania na anajivunia kuwa Mtanzania japo ana asili ya India.

Mbunifu huyo wa jina la Tanzania ni Mhandisi wa Masuala ya Redio, kazi anayoifanya nchini Uingereza, akieleza kuwa katika kuienzi nchi yake, nyumba yake iliyopo mjini Birmingham, ameipa jina la Dar es Salaam, ikiwakilisha ubini wake, pamoja na Jiji la Dar es Salaam.

Mohammed Iqbal Dar kwa sasa anaishi Uingereza kwa kuwa huko ndiko alikopata kazi eneo la Birmigham b35 6ps UK, Dar –es-Salaam House, 18 TURNHOUSE ROAD,PHONE 44 121-747-9822.

Imeandaliwa na: James J. Waibina 
kwa msaada wa Mtandao.

Kwa Maoni /Ushauri : 0713 515059 -(WhatsApp)
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

1 blogger-facebook:

  1. Imekaa vizuri mungu aendelee kumbariki kws kuipa nchi yetu jina zuri

    ReplyDelete

Item Reviewed: Mfahamu Mwasisi wa Jina la “TANZANIA” na jinsi alivyobuni jina hilo. Rating: 5 Reviewed By: Unknown